Ndugu Wanahabari,
Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa TAKUKURU ni chombo chenye dhamana ya kusimamia Mapambano Dhidi ya Rushwa nchini kwa mujibu wa Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Na. 11 ya Mwaka 2007 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2019. Tunakutana na ninyi waandishi ili kupitia kwenu, tuuhabarishe umma kuhusu utendaji kazi wetu kama ambavyo imekuwa ikifanyika kila robo ya mwaka. Taarifa inayowasilishwa leo, inahusu utendaji kazi wa ofisi yetu katika maeneo yote matatu yaani Uchunguzi, Elimu kwa Umma na Uzuiaji wa Vitendo vya Rushwa kwa kipindi cha Oktoba – Disemba 2021.
Ndugu Wanahabari,
Katika Dawati la Uchunguzi kwa kipindi cha Oktoba hadi Desemba, 2021 TAKUKURU Mkoa wa Singida imetekeleza majukumu yafuatayo:-
- Jumla ya taarifa au malalamiko 101 yalipokelewa ambapo taarifa 63 zilihusu vitendo vya rushwa na taarifa 38 hazikuhusu vitendo vya rushwa.
Mchanganuo wa malalamiko hayo 101 yaliyopokelewa kisekta ni kama ifuatavyo:
TAMISEMI 44, Afya 14, Ardhi 13, Mahakama 08, Polisi 06, Elimu 04, Binafsi 03, Fedha 03, Kilimo 01, Manunuzi 01, Maliasili 01, Maji 01, Nishati 01 na Mifuko ya hifadhi ya jamii 01.
- Malalamiko 63 yaliyohusu rushwa uchunguzi wake unaendelea katika hatua mbalimbali na Malalamiko 38 ambayo yalibainika hayahusiani na rushwa walalamikaji walipewa ushauri na kuhamishiwa idara nyingine kwa hatua zaidi.
- Katika kipindi husika, jumla ya kesi tatu (03) zilifunguliwa Mahakamani na kufanya jumla ya kesi zinazoendelea mahakamani kuwa kumi na tano (15).
- Katika kipindi hiki cha Oktoba – Desemba 2021, Kesi 6 zilitolewa uamuzi mahakamani na Jamhuri ilishinda katika kesi zote.
Ndugu Wanahabari,
Elimu kwa Umma: Elimu kwa umma inafanyika ili kuielimisha jamii kuhusu madhara ya rushwa kwa jamii na Taifa kwa ujumla. Elimu kwa umma pia inafanyika kwa madhumuni ya kuipa jamii uelewa na hivyo kuihamasisha jamii kushiriki kikamilifu katika mapambano dhidi ya rushwa.
TAKUKURU mkoa wa Singida kupitia Dawati la Elimu kwa Umma hutumia mbinu mbalimbali katika kuelimisha kwa kuwashirikisha wanajamii wa makundi mbalimbali ikiwa ni pamoja na vijana wa shule za Msingi, Sekondari, Vyuo, Watumishi wa Umma na jamii kwa ujumla.
TAKUKURU Mkoa wa Singida kwa kushirikiana na Chama cha SKAUTI Tanzania, imefanikiwa kuanzisha ummoja unaojulikana kwa jina la TAKUKURU – SKAUTI [TAKUSKA]. Walezi wa ummoja huu ni Wakuu wa Mikoa kwa ngazi ya mkoa na Wakuu wa Wilaya kwa ngazi ya wilaya na mwongozo umetolewa wa mashirikiano kati ya TAKUKURU na Skauti.
Mwongozo huo ambao ni MWONGOZO WA MAFUNZO KWA WAWEZESHAJI WA KUFUNDISHIA VIJANA WA SKAUTI KUHUSU KUZUIA NA KUPAMBANA NA RUSHWA, ulizinduliwa kitaifa na baadaye kutambulishwa katika ngazi ya mkoa na wilaya zote za Mkoa wa Singida. Mwongozo huu utatumika katika uelimishaji kwa lengo la kujumuisha vijana wa Skauti katika mapambano dhidi ya Rushwa.
Vilevile, kwa kipindi cha mwezi Oktoba hadi Disemba, 2021, jumla ya mikutano ya hadhara 24 imefanyika, semina 32 zimefanyika, klabu za wapinga Rushwa 58 zimeimarishwa na vipindi vya Redio 02 vilirushwa kupitia Standard Radio Fm ya mkoani Singida.
Ndugu Wanahabari,
Pia TAKUKURU INAYOTEMBEA ilitembelea Chuo cha Uuguzi Kiomboi (Kiomboi School of Nursing – KNTC) kilichopo Wilaya ya Iramba kwa lengo la kuwaelimisha na kupokea kero mbalimbali kuhusu Rushwa. Kupitia uelimishaji huo, tulipokea malalamiko kwamba, baadhi ya Wanachuo wanaofadhiliwa na Shirika lisilo la Kiserikali la Ufadhili wa Masomo kwa watoto wa kike wanaoishi katika mazingira magumu -CAMFED walilalamika kuwa, baada ya kuingiziwa fedha za kujikimu kwenye akaunti zao za benki, Uongozi wa chuo uliwaamuru wanachuo hao kutoa kwa uongozi wa Chuo, fedha kiasi cha Sh. 720,000/= kinyume na utaratibu wa Chuo pamoja na shirika la CAMFED. Baada ya TAKUKURU Mkoa wa Singida kupitia sheria na taratibu za chuo, ilibainika kuwa wanachuo hao hawakutakiwa kufanya hivyo na iliamuliwa kuwa kila mwanachuo aliyetoa fedha Sh. 720,000/= kwa uongozi wa chuo, basi arudishiwe fedha hizo.
Ndugu Wanahabari,
Uzuiaji Vitendo vya Rushwa ni jukumu moja wapo linalotekelezwa na TAKUKURU kwa madhumuni ya kuzuia athari ambazo jamii ingezipata kama vitendo vya rushwa vingeachwa vikatokea. Ili kudhibiti mianya ya rushwa katika Idara mbalimbali, TAKUKURU (M) Singida imefanya kazi ya uchambuzi wa mifumo kwa lengo la kubaini mianya ya rushwa. TAKUKURU mkoa wa Singida imefanya uchambuzi wa mifumo mbali mbali ili kubaini mapungufu katika maeneo yafuatayo:-
- Uchambuzi wa mfumo wa manunuzi yanayofanyika kupitia Wakala wa Huduma ya Ununuzi Serikalini – GPSA ambapo lengo lilikuwa ni kubaini mianya ya rushwa katika eneo hili ambalo wadau wamekuwa wakililalamikia.
- Kwa kipindi hicho pia ulifanyika uchambuzi wa mfumo juu ya athari za rushwa ya Ngono katika tasisi za elimu kuanzia elimu ya Msingi, Sekondari pamoja Vyuo vikuu vilivyopo Mkoa wa Singida.
Kupitia chambuzi hizi, mapungufu yanayopelekea mianya ya rushwa yalibainishwa na hivyo kwa robo ya tatu TAKUKURU itafanya warsha na wadau husika kujadili matokeo ya chambuzi hizi na kuwekeana maazimio ya namna bora ya kuondokana na mianya hiyo ya rushwa katika maeneo yao ya kazi.
Ndugu Wanahabari,
Katika Miradi ya Maendeleo, katika kipindi tajwa tuliendelea kufuatilia miradi mbali mbali ya maendeleo ambapo malengo ya kufanya ufuatiliaji huo yalikuwa kama ifuatavyo:
- Kujenga uelewa wa pamoja kuhusu kiasi cha fedha kilichotengwa kwa ajili ya miradi ya ujenzi, ukarabati wa barabara, afya, elimu, maji n.k iliyopo chini ya Mamlaka za Serikali za mitaa, Wakala wa Serikali na Serikali Kuu, kwa nia ya kuona uwiano kati ya matumizi ya fedha za umma na ubora wa huduma zinazotolewa,
- Kuimarisha uwazi na uwajibikaji katika mchakato wa utekelezaji wa bajeti,
- Kuimarisha ufanisi na matokeo mazuri ya matumizi ya fedha za umma na kupata msingi wa kufanya udhibiti na ufuatiliaji wa utekelezaji wa bajeti katika miradi husika.
Aidha katika kipindi cha Oktoba hadi Disemba 2021 TAKUKURU (M) Singida ilifanya ufuatiliaji wa Miradi ya Maendeleo Saba (07) katika maeneo yafuatayo. Afya mradi 01 wenye thamani ya shs, 250,000,000.00/=; Maji miradi 02 yenye thamani ya shs, 960,651,113/=; Elimu mmoja (01) Bweni lenye thamani ya Tsh 80,000,000/=. Jumla miradi yote iliyokaguliwa ilikuwa na thamani ya shs, 1,290,651,113/=.
Mapungufu yaliyobainika katika Ukaguzi wa miradi hiyo ambayo yangeweza kusababisha mianya ya rushwa, yameweza kufanyiwa kazi kwa kutoa elimu kwa lengo la kuondoa mianya ya rushwa iliyopo na kuimarisha usimamizi wa miradi kwa kusisitiza uzingatiaji wa sheria na kanuni za manunuzi ya umma ili kupata miradi bora yenye kukidhi thamani ya fedha (Value for money).
Ndugu Wanahabari,
Katika hatua nyingine, mtakumbuka kuwa Mwezi Oktoba Mwaka jana, Serikali ilileta katika Mkoa wa Singida fedha za Mpango wa Maendeleo ya Ustawi wa Taifa na Mapambano Dhidi ya UVIKO-19 ambazo zilipokelewa katika Halmashauri zilizopo mkoa wa Singida. Fedha hizo zilitengwa kwa matumizi ya ujenzi wa madarasa. Napenda kuwataarifu kuwa TAKUKURU ilifuatilia fedha hizi kuanzia hatua ya Ununuzi, ujenzi hadi ukamilishaji. Katika ufuatiliaji huo Halmashauri zote sita zimekamilisha ujenzi wa madarasa hayo kwa asilimia mia moja (100%) na Halmashauri ya Itigi ujenzi wa Madarasa hayo upo katika hatua ya ukamilishaji na wasimamizi wamehahidi kuwa kabla Mwezi wa kwanza kuisha ujenzi utakuwa umekamilika.
Ndugu Wanahabari,
Mkakati wa utendaji kazi TAKUKURU (M) Singida kwa robo ya tatu ya mwaka 2021/2022 inayoanzia Januari hadi Machi 2022 ni kufuatilia matumizi ya fedha za Serikali zinazoelekezwa Mkoa wa Singida kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo; kufanya uchunguzi pale itakapobainika kuwa katika ufuatiliaji huo wa matumizi ya fedha za Serikali zinazoelekezwa Mkoa wa Singida vitendo vya rushwa vimejitokeza; na kuendelea na uelimishaji unaolenga kushirikisha jamii katika mapambano dhidi ya rushwa ikiwa ni pamoja na kuendelea kutekeleza Mpango Kazi wa TAKUSKA.
Ndugu Wanahabari,
TAKUKURU (M) inatoa rai kwa wananchi wote kwa ujumla kujiepusha na vitendo vya Rushwa na kushiriki kikamilifu katika vita dhidi ya rushwa kwa kutoa taarifa za vitendo vya Rushwa kwa njia mbalimbali ikiwemo:-
- Kufika Ofisi za TAKUKURU (M) na Wilaya;
- Kupiga simu namba 113 au kupiga simu kwa Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Singida kwa Namba 0738-150-208;
- Kutumia TAKUKURU APP hasa kwa Rushwa za barabarani pale wanapobaini kutokea/kutaka kutokea kwa vitendo vya Rushwa;
- Kutoa ushirikiano kwenye uchunguzi na kushiriki kutoa ushahidi Mahakamani.
Ndugu Wanahabari,
Katika Mkoa wa Singida, kama ilivyo kwa mikoa mingine, kumekuwepo na wimbi la watu wanaojifanya Maafisa wa TAKUKURU na kujipatia fedha kwa kuwahadaa kuwa wanaweza kuwasaidia kupata huduma au nafuu zozote kutoka mamlaka mbalimbali za Serikali.
TAKUKURU (M) Singida inawataadharisha wale wote wanaowatapeli au wanaopanga kuwatapeli wananchi kwa kujifanya Maafisa wa TAKUKURU au vyombo vingine vya dola kuacha kwa sababu watakapobainika hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao ikiwemo kuwafikisha Mahakamani.
Imetolewa na:
imesainiwa
MZALENDO WIDEGE
MKUU WA TAKUKURU (M)
SINGIDA
SIMU: 0738150208